Saturday, January 26, 2013

MTAWA WA KANISA APORA MUME WA MTU, SASA KUBURUZWA MAHAKAMANI

KESI ya madai inayomkabili aliyekuwa Mtawa wa Shirika la Kitawa la Kanisa Katoliki Jimbo la Sumbawanga, Sista Yasinta Sindani anayedaiwa kufumaniwa na mume wa mtu imepangwa kusikilizwa Januari 29 mwaka huu.

“Sista’ Yasita licha ya kuwa mtumishi wa afya katika Hospitali ya Mkoa wa Rukwa mjini hapa lakini inadaiwa ameachana na maisha ya kitawa miaka miwili iliyopita kwa hiyari yake akiwa Mtawa wa Shirika la Masista wa Maria Mtakatifu Malkia wa Afrika (MMMA).

Shauri hilo la madai linatarajiwa kuanza kusikiliza katika Mahakama ya Mwanzo mjini hapa, mbele ya Hakimu Jaffari Mkinga, mlalamikaji Asteria Mgabo anamtaka Yasinta amlipe Sh3 milioni baada ya kumfumania na mumewe wa ndoa aitwaye Martin Msangawale (39), Mhasibu wa Manispaa ya Sumbawanga.

Siku hiyo ya kusikilizwa kwa shauri hilo mlalamikaji katika shauri hilo Asteria anatarajiwa kuwaleta mashahidi wake wanne mahakamani hapo.

Katika hati ya awali ya madai inadaiwa kuwa mshtakiwa alifumaniwa na Asteria akiwa na mumewe Msangawale wakiwa kwenye nyumba ya kulala wageni ya Chipu iliyoko eneo la Katandala mjini Sumbawanga usiku wa Desemba 24 mwaka jana siku ya mkesha wa Sikukuu ya Krismasi. Hakimu, Mkinga alisema kuwa kesi hiyo iliyokuwa isikilizwe Januari 21 imeahirishwa hadi Januari 29 mwaka huu ili kumapatia mlalamikaji muda wa kuwaleta mashahidi wake mahakamani.

Mlalamikaji wa shauri hilo la madai, Asteria amedai nje ya mahakama kuwa alifunga ndoa ya Kikristu na mumewe huyo Martin Msangawale mwaka 2007.
Kesi hiyo inatarajiwa kuvuta hisia za watu wengi hususani wakazi wa Manispaa ya Sumbawanga na vitongoji vyake kutokana na kuwa gumzo kubwa na kuteka hisia za watu wengi hivi sasa.

MWANANCHI

No comments:

Post a Comment