Friday, January 18, 2013

MSHIRIKA WA GBAGBO AKAMATWA GHANA

Aliyekuwa waziri matata wa vijana na mshirika mkubwa wa aliyekuwa rais Laurent Gbagbo, Charles Ble Goude, amekamatwa nchini Ghana. Bwana Ble Goude anakanusha madai ya kuongoza wapiganaji waliowashambulia raia wa kigeni na raia kutoka Kaskazini mwa nchi wakati wa uchaguzi uliokumbwa na utata mwaka 2010. Amekuwa mafichoni tangu Aprili mwaka 2011, wakati Gbagbo alipokamatwa.
Gbagbo anasubiri kusikilizwa kwa kesi yake katika mahakama ya kimataifa ya jinai huko Hague akikabiliwa na makosa ya uhalifu dhidi ya binadamu.
Watu elfu tatu walipoteza maisha yao katika mzozo huo uliodumu miezi minne wakati Gbagbo alikataa kuondoka mamlakani baada ya kushindwa.
Washirika kadhaa wa Gbagbo wamekimbilia uhamishoni nchini Ghana na mwanzo waliripoti kuwa bwana Ble Goude amekamatwa.
"naweza kuthibitisha kuwa tumemkamata mtu tunaye amini kuwa waziri wa zamani wa vijana nchini Ivory Coast.'' alisema Larry Gbevlo-Lartey, katibu wa usalama.
"kuna waranti ya kumkamata na tumekuwa tukimsaka kwa muda mrefu sana. Tungali tunatafuta habari zaidi na kisha tutaweza kumkabidhi kwa serikali,'' aliongeza katibu huyo.
Mwaka jana aliambia BBC kuwa kama kiongozi wa vijana yeye aliandaa tu mikutano ya hadhara na wala hakuwahi kuwa kiongoizi wa wapiganaji.
"mimi sio kiongozi wa wapiganaji, sijawahi kununua silaha tullifanya maandamano dhidi ya wale waliokuwa na silaha, hatukuwa tumebeba chochote,'' alisema Ble Goude
Alisema kuwa yuko tayari kwenda katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita kujiondolea lawama.
Bwana Ble Goude aliwekewa vikwazo na Umoja wa mataifa mwaka 2006 akituhumiwa kwa kuchochea mashambulizi dhidi ya maafisa wa umoja huo.
Chanzo - BBC Swahili

No comments:

Post a Comment