Friday, January 18, 2013

TPA YASUASUA KUITIMUA MELI ILIYOBEBA MAFUTA MACHAFU

Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imeshindwa kueleza kama imetekeleza agizo la Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, kuhakikisha inaiondoa meli ya Mt. Al Biraq katika ardhi ya Tanzania ndani ya saa 24. Meli hiyo yenye namba za usajili IMO 9381732 iliamriwa kuondoka nchini juzi kutokana na kuingiza mafuta ya dizeli ambayo hayana viwango vya ubora. Mfuta hayo ambayo ni tani 100,010 yalibainika kuwa hayafai baada ya Shirika la Taifa la Viwango Tanzania (TBS) kuyapima na kubaini hayana viwango vya ubora.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Madeni Kipande, akizungumza na NIPASHE jana kama agizo la Waziri limetekelezwa, alisema kiutaratibu meli inakuwa chini ya uangalizi wa TPA pale inapokuwa ndani ya bandari.
Kipande hata hivyo, hakuweza kufafanua kama anamaanisha kuwa meli hiyo haikuwa ndani ya bandari, alisema agizo la waziri atakaporudi ofisini kwake ataliangalia.
“Kwa kuwa nipo nje ya ofisi, nikirudi ofisini nitaliangalia na kukupigia simu kukujulisha,” alisema Kipande.
Hata hivyo, baadaye  NIPASHE ilipomtafuta Kipande kwa kumpigiwa simu, alijibu kwa kifupi kuwa hana muda wa kuelezea suala la meli na kukata simu.  
Awali Kipande alisema kurejea kwa meli hiyo ikiwa na shehena ya mafuta yaliyokataliwa mwaka jana kulisababisha  mvutano baina ya baadhi ya taasisi.
Juzi Dk. Mwakyembe alisema meli hiyo  iliwasili nchini Desemba 27, mwaka jana ikiwa na shehena ya tani 100,010 ya dizeli, lakini ikagundulika kuwa mafuta hayo hayana ubora na kutakiwa kurejea nayo yalikotoka.
Siku tisa baadaye yaani Januari 5, mwaka huu ilirejea nchini ikiwa na shehena ile ile kwa nia ya kudanganya mamlaka za Tanzania ili kuruhusiwa kuuza mafuta katika soko la Tanzania.
Alisema kuwa Januari 15, mwaka huu meli hiyo baada ya kuingiza mafuta hayo yalipimwa na TBS na kukuta matatizo yale yale na hivyo kuagiza yasiingizwe nchini kutokana na kuwa chini ya viwango vya ubora.

No comments:

Post a Comment