Kituo cha
Sheria kwa Wanawake na Maendeleo ya Afrika (WiLDAF) kimesema kitendo cha
wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) kubakwa na kulawitiwa
kinatokana na uzembe wa Serikali kutokuwa na bodi ya kusimamia ujenzi wa
hosteli za wanafunzi ikiwa ni pamoja na kujenga ukuta mrefu na kuwa na
walinzi wa kutosha.
Mkurugenzi
wa kituo hicho, Dk. Judith Odunga, alisema jijini Dar es Salaam kuwa
Serikali ilitakiwa kuweka bodi itakayosimamia ujenzi wa mabweni ya
wasichana na wavulana tena kwa kiwango kinachotakiwa kisheria ikiwa ni
pamoja na kujenga uzio mkubwa na kuweka walinzi wakutosha ili kuepuka
madhara kama yaliyotokea kwa wanafunzi wa chuo hicho kilichoko katikati
ya Jiji la Dar es Salaam.
“Jambo hili
limeniuma sana na limetokana na uzembe wa serikali kutosimamia vema
wamiliki wa hosteli kuwapa masharti ya ujenzi wa hosteli za wanafunzi,”
alisema.
Dk. Odunga
alisema kuwa serikali inatakiwa kuwasimamia wamiliki wa hosteli ili
vitendo vya wanafunzi kupigwa, kuibiwa, kulawitiwa na kubakwa
kutojirudia tena katika hosteli zinazotumiwa na wanafunzi wa vyuo vikuu
vingine.
Dk. Odunga
pia alilaani kitendo cha baadhi ya askari polisi kutumia nguvu kubwa
kuwatawanya wanafunzi kwa kuwapiga wakitumia viboko na mabomu na
kusababisha baadhi yao kuzirai.
Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, kitendo hicho kinakiuka haki za binadamu kwa kuwa binadamu ana haki ya kusikilizwa.
Jumatatu
wiki hii, wanafunzi wa IFM walifanya maandamano makubwa jijini Dar es
Salaam hadi katika ofisi za Makao Makuu ya Jeshi la Polisi na Makao
Makuu ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi wakilalamikia Jeshi hilo kwa
kushindwa kuchukua hatua dhidi ya vitendo vya wizi, kulawitiwa na
kubakwa, ambavyo wanafanyiwa na genge la wahuni katika hosteli yao
iliyoko Kigamboni.
CHANZO: NIPASHE
No comments:
Post a Comment